Sunday, March 8, 2015

USAFI WA ZITTO KABWE

Kuna kashfa inaenda na kujirudia kuwa Bwana Zitto Zuberi Kabwe (Mwanasiasa msafi kuliko wanasiasa wote kuwahi kutokea Tanzania)  ni moja ya watu walionufaika na mgao wa fedha za escrow, japo sijawahi msikia akitamka kwa ulimi wake kuwa hajapokea, ameishia kusema watu wachunguze, nitaendelea kuamini katika misingi ya mtu ni huru mpaka pale itakapothibitika kua ana makosa.

Lakini kaka yangu huyu amekuwa ni mtaalamu mzuri wa matumizi ya "fallacy" kwa waliosoma falsafa wataelewa. Zinapozuka kashfa dhidi yake, huwa anatumia A kujibu swali B. tundu lissu alipomkashifu kwa kupokea pesa toka kwa Mkono na mpaka sasa ana miliki magari mawili ya Mkono, Bwana Zitto aliishia kuhamishia kashfa kwa Mh  Mbowe, na kusema haongei na kifaranga yaani Lissu, hii kwenye falsafa inaitwa appeal to mockery ab absurdo

lakini pia mbinu nyengine mheshimiwa hutumia ni Argumentum ad misericordiam au kwa lugha nyepesi appeal to pity (inatafsiriwa kama kuweza kushinda mjadala kwa kuvuta hisia na huruma ya walio wengi)  Ilipozuka kashfa kuwa bwana zitto kabwe kuna ufisadi anafanya kupitia kampuni ya Gombe advisors, Bwana zitto alijibu ameumizwa sana kwa kuwa yupo busy anamuuguza mama ( Mwenyezimungu amlaze mahala pema Peponi aamin) ilipoibuka tena bungeni kashfa ya kupokea hela za escrow alisema tumuache mama apumzike kwa amani.

Lakini kwa kuwa vifaranga vimekuwa, na hana anayemuuguza, tunaomba sasa atujibu kwa ufasaha kwa kuwa maelezo yake ya awali yalijaa na uuguzi,  kuhusu mikataba wa leka Dutigite kwa upande mmoja na NSSF na TANAPA kwa upande mwengine

Kampuni ya Leka Dutigite ina wana hisa 16, 15 kati yao ni wasanii wa kizazi kipya wenye hisa asilimia 5 kila mmoja hivyo kuwa idadi ya asilimia 75 na asilimia 25 zilizobakia zinamilikiwa na Gombe advisors. Swali huyu Gombe ni nani?

Ukienda kuangalia makabrasha ya Brela Gombe advisors inamilikiwa na watu wawili, mtu mmoja mwenye jina la kikenya mwenye asilimia 25 na Bwana Zitto kabwe ambae kwenye fomu amejijaza kama mchumi badala ya kiongozi wa Umma

Kwa hiyo kumbe NSSF na TANAPA mashirika ya Umma ambayo yanakaguliwa yasifanye ufisadi na Bwana Zitto kabwe kwa mkono wa kulia, ukija mkono wa kushoto unakuta Bwana Zitto kabwe ndo mwanahisa mkuu kwenye mikataba ya kibiashara baina ya NSSF, TANAPA na leka dutigite, japo yeye anadai hakuna mgongano wa kimaslahi.

Katika tenda moja, NSSF iliilipa Leka Dutigite shilingi milioni 120, milioni 90 kati ya hizo zilitolewa siku moja baada ya kuwekwa, siku moja kabla ya uchaguzi wa kamati ya hesabu za mashirika ya umma PAC uliomfanya Bwana Zitto kuwa mwenyekiti wa kamati na kumng'oa mzee Cheyo aliyekuwa anafanya kazi kwa weledi mkubwa. Coincidence? ipo siku utawala utabadilika na hizi pesa zitamulikwa

Na ni bahati nzuri kuwa hizo pesa zilienda kutolewa na Habib Mchange, (bank statement inaeleza hivyo) aliyefukuzwa Chadema kwa kosa la kuwa kibaraka wa Zitto na kupanga mapinduzi ndani ya Chama, leo ndio katibu mkuu wa LekaDutigite kampuni ambayo Zitto anasema hana maslahi humo, kwa nini aweke watu wake?

Sasa hapa kuna maswali yanajitokeza

1. je NSSF na TANAPA ni mashirika ya Umma au hapana? Na je Zitto ni kiongozi wa Umma au Hapana

2. je Zitto anayakagua haya mashirika au hapana?

3. Je katiba ya jamhuri ya muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 sura ya 6 sehemu ya 2 Na sheria ya utumishi wa Umma inamruhusu kiongozi kama yeye kuingia mkataba na mashirika ya Umma ukiachila mbali mashirika yanayoripoti chini yake?

4. Kama Gombe advisors si kampuni ya faida, kwa nini ijimilikishe hisa asilimia 25% Za Leka Dutigite? Je si ingekuwa sahihi ingebaki kuwa mshauri tu na wasanii wakagawana asilimia 100 ya kampuni ili wanapogawana faida wagawane kwa uwiano sawa kutokana na mgawanyo wa hisa zao

5. Kwa nini aweke watu wake wa karibu kuwa ndio viongozi wa Leka Dutigite kama yeye ni mdhamini tu na mshauri wa wanamuziki?

Mimi naamini hakuna ujanja ujanja unaodumu kwa muda mrefu nchi hii kabla haujagundulika, Chama Chake kimeshamjua, ipo siku hao anaowatumia kwenye ujanja ujanja wake watamgeuke na ukweli utawekwa hadharani. lakini hadi hapo yatakoapotokea hayo, bado nasubiri siku nione Zitto Kabwe akiikosoa NSSF na TANAPA kwa kuwa mpaka sasa kila akiongea mifano mema hutolea mashirika haya mawili. Mimi ndio yule yule niliyemtabiria kufukuzwa kwenye chama siku
aliyochaguliwa kuwa kiongozi wa chama.